• HABARI MPYA

    Wednesday, April 16, 2014

    HANS POPPE AOKOA JAHAZI SIMBA SC, WACHEZAJI WALIGOMA KWENDA KAMBINI ZANZIBAR AKAMWAGA MPUNGA...SASA SHWARI, YANGA WAJIPANGE ‘FETE FETE’ LA JUMAMOSI

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    WACHEZAJI 18  wa Simba SC wanaingia kambini leo visiwani Zanzibar kwa ajili ya mchezo dhidi ya mahasimu, Yanga SC Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kufunga pazia la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Hata hivyo, wachezaji hao waliutikisa uongozi wao asubuhi ya leo baada ya kugoma kwenda Zanzibar hadi kwanza wapewe mishahara yao ya mwezi huu jambo ambalo liliwafanya viongozi wa timu hiyo wahangaike hadi kupata fedha hizo na kuwalipa.
    Mkombozi daima; Hans Poppe ameendelea kuwa mtu muhimu Simba SC baada ya kuokoa jahazi leo
    Kambini Zanzibar; Kikosi cha Simba kinaingia kambini visiwani Zanzibar leo tayari kwa mchezo na Yanga Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Aliyeokoa jahazi hilo si mwingine zaidi ya Zacharia Hans Poppe, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili na kipenzi cha wana Simba SC ambaye amelipa mishahara yote, kuanzia wachezaji hadi benchi la Ufundi na akawaambia; “Nataka mtafune kandambili Jumamosi”.
    Kocha Msaidizi wa Simba SC, Suleiman Abdallah Matola ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba kikosi cha wachezaji 18 na benchi zima la Ufundi kinaingia kambini Zanzibar leo kumkusanyia nguvu mtani.
    Nahodha huyo wa zamani wa Simba na kiungo mahiri enzi zake, amesema wachezaji wanakwenda Zanzibar wakiwa na morali ya hali ya juu na anaamini Jumapili wataifanya Yanga ile kitu wapenzi wa Simba wanapenda.
    Matola amewataja wachezaji wanaokwenda kambini ni makipa; Ivo Mapunda na Yaw Berko, mabeki William Lucian ‘Gallas’, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ Joseph Owino, Donald Mosoti, Nassor Masoud ‘Chollo’, viungo Henry Joseph, Ramadhani Chombo ‘Redondo’, Uhuru Suleiman Jonas Mkude, Said Ndemla, Awadh Juma, Ramadhani Singano ‘Mesi’, Haroun Chanongo, Amri Kiemba na washambuliaji Amisi Tambwe na Zahor Pazi.
    Matola enzi zake akiitwa Veron akifananishwa na kiungo wa zamani wa kimataifa wa Argentina, Juan Sebastian Veron amesema kikosi hicho kitakuwa visiwani Zanzibar hadi Jumamosi kitakaporejea na moja kwa moja kuelekea Uwanja wa Taifa.
    Simba na Yanga zinakutana Jumamosi katika mchezo wa mwisho wa ligi ambao hautakuwa na mchecheto kwa sababu hautabadili chochote katika msimamo wa Ligi Kuu, kwa kuwa tayari bingwa, mshindi wa pili na wa tatu wamekwishapatikana.
    Azam imejihakikishia ubingwa kwa kufikisha pointi 59 ikiwa na mchezo mmoja mkononi ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote baada ya mechi za mwisho Jumamosi, wakati Yanga SC yenye pointi 55 sasa ikiifunga Simba SC itafikisha 58 na kubaki nafasi ya pili tu, huku Mbeya City yenye pointi 46 ni ya tatu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HANS POPPE AOKOA JAHAZI SIMBA SC, WACHEZAJI WALIGOMA KWENDA KAMBINI ZANZIBAR AKAMWAGA MPUNGA...SASA SHWARI, YANGA WAJIPANGE ‘FETE FETE’ LA JUMAMOSI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top