• HABARI MPYA

    Wednesday, November 26, 2014

    SIMBA SC WAINGIA VITANI NA GOR MAHIA KUWANIA SAINI YA MFUNGAJI BORA KENYA

    Na Vincent Malouda, NAIROBI
    YULE mchezaji ambaye Simba SC wanamtaka, Dan Sserunkuma yuko kwenye mazungumzo na klabu yake, Gor Mahia ili aongeze Mkataba.
    Katibu Mkuu wa Gor Mahia, Chris Omondi amesema leo mjini Nairobi kwamba wameanza mazungumzo na mfungaji huyo bora wa Ligi Kuu ya Kenya ambaye anachezea timu ya taifa ya Uganda, The Cranes ili abaki.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY mjini Nairobi leo mchana, Omondi amesema kwamba Sserunkuma ameonyesha dalili za kutosha za kutaka kubaki na mabingwa hao wa Kenya 2014. 
    Ni Simba SC, au atabaki Gor Mahia; Mshambuliaji Dan Sserunkuma yuko katikati ya njia mbili, kwenda Dar es Salaam au kubaki Nairobi

    “Tupo kwenye mazungumzo naye na ameonyesha dhamira ya kubaki na sisi. Anafahamu nini kipo mezani, na tunajua thamani yake, hivyo hapo ndipo tulipo,”amesema.
    Sserunkuma, ambaye alijiunga na Gor Mahia akitokea Nairobi City Stars katikati ya mwaka 2012-  amekuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Kenya kwa mabao yake 16, akiiwezesha timu hiyo kutetea taji.
    Mjini Dar es Salaam kumekuwa na habari kwamba, mchezaji huyo anatakiwa na Simba SC, ingawa Rais wa klabu hiyo Evans Aveva alikaririwa na BIN ZUBEIRY akisema hawahitaji mshambuliaji wa kigeni kwa msimu huu.
    Tayari kikosini Simba SC ina wachezaji watano wa kigeni ambao ni idadi kamili kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu Tanzania- hao ni Waganda beki Joseph Owino, mshambuliaji Emannuel Okwi, Warundi kiungo Pierre Kwizera na mshambuliaji Amisi Tambwe pamoja na Mkenya, mshambuliaji Paul Kiongera.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC WAINGIA VITANI NA GOR MAHIA KUWANIA SAINI YA MFUNGAJI BORA KENYA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top