• HABARI MPYA

    Wednesday, April 01, 2015

    HABARI NJEMA AZAM FC, KIPRE MICHAEL BALOU SASA FITI KABISA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KIUNGO mkabaji wa Azam FC, Kipre Michael Balou anatarajiwa kurejea uwanjani wiki ijayo, baada ya kukosekana kwa wiki tatu kutokana na maumivu ya msuli wa paja la kulia.
    Meneja wa Azam FC, Jemadari Said Kazumari ameiambia BIN ZUBEIRY leo mjini Dar es Salaam kwamba, Balou ana siku tatu sasa tangu aanze programu kamili ya mazoezi.
    Mshambuliaji huyo wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, aliyewika Kariakoo United ya Lindi ikiwa Ligi Kuu, amesema Balou kwa sasa amepona kabisa na yuko tayari kurudi uwanjani.
    “Habari njema ni kwamba kiungo wetu tegemeo mkabaji, Kipre Balou amepona kabisa na ameanza mazoezi, maana yake yuko tayari kurudi kazini wiki ijayo,”amesema.
    Kipre Balou juu anatarajiwa kurejea wiki ijayo kikosini Azam FC

    Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, wanaendelea na mazoezi Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam kujiandaa na mechi dhidi ya Mbeya City Jumatano ijayo.
    Azam FC wataikaribisha Mbeya City Aprili 8, Uwanja wa Azam Complex katika mfululizo wa Ligi Kuu, huo ukiwa mchezo wa marudiano baada ya awali timu hiyo ya Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na familia yake kushinda 1-0 Uwanja wa Sokoine, Mbeya.
    Mbali na Balou, raia wa Ivory Coast aliyetua Chamazi miaka mitatu iliyopita, majeruhi wengine ambao bado wanajiuguza ni kiungo mshambuliaji Khamis Mcha ‘Vialli’ anayesumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu sawa na beki wa pembeni, Waziri Salum.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HABARI NJEMA AZAM FC, KIPRE MICHAEL BALOU SASA FITI KABISA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top