• HABARI MPYA

    Thursday, April 02, 2015

    STRAIKA NA MIDO HATARI PLATINUM WALIOIKOSA YANGA DAR, SASA WAPO FITI KWA MCHEZO WA MARUDIANO JUMAMOSI MANDAVA

    Na Mwandishi Wetu, BULAWAYO
    KOCHA wa FC Platinum ya Zimbabwe, Norman Mapeza amepokea ahueni kuelekea mchezo wa marudiano hatua ya 32 Bora Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Yanga SC ya Tanzania.
    Hiyo inafuatia wachezaji wake wawili walioukosa mchezo wa kwanza Dar es Salaam wiki mbili zilizopita, kiungo Wisdom Mutasa aliyekuwa anasumbuliwa na mafua na mshambuliaji Donald Ngoma aliyekuwa majeruhi kurejea uwanjani.
    Wawili hao, wote wanaendelea na mazoezi na wenzao- na Mutasa anatarajiwa kuongeza ubunifu katika eneo la katikati ya Uwanja, wakati Ngoma anatarajiwa kuongeza ufanisi wa upatikanaji wa mabao Jumamosi.
    Donald Ngoma atacheza Jumamosi Mandava, baada ya kuukosa mchezo wa kwanza Dar es Salaam

    Platinum watatakiwa kuupanda mlima kama wanataka kusonga mbele michuano hiyo ya pili kwa ukubwa kwa klabu barani, kufuatia awali kufungwa 5-1 na Yanga.
    Ushindi wa mabao 4-0 Uwanja wa Mandava keshokutwa utaifanya timu hiyo yenye maskani yake Zvishavane iitoe Yanga SC kwa faida ya bao la ugenini.
    Kikosi cha kocha Norman Mapeza kimekuwa na wakati mgumu siku za karibuni, baada ya kulazimishwa sare ya 2-2 nyumbani na timu mpya Ligi Kuu ya Zimbabwe, Dongo Sawmills kabla ya kufungwa 1-0 na Caps United mjini Harare Jumapili iliyopita.
    Pamoja na hayo, Mapeza hataki kukataa tamaa, akisema kwamba watacheza mchezo wao wa kawaida dhidi ya Yanga SC ili kuangalia mustakabali baada ya dakika 90.
    "Tunafahamu nini tunahitaji kufanya, lakini hatutaki kujitia presha. Tutakwenda kucheza mchezo wetu wa kawaida, ili tuone mambo yatakuwaje baada ya dakika 90,” amesema.
    Yanga SC wamekuwa katika wimbi zuri la ushindi tangu waifunge Platinum, wakitoka kufungwa 1-0 na mahasimu, Simba SC- kwani tangu hapo wameifunga Kagera Sugar 2-1, JKT Mgambo 2-0 na JKT Ruvu 3-1.
    Kikosi cha Yanga SC kinatarajiwa kuondoka Dar es Salaam kesho kwa ndege maalum ya kukodi, ya Serikali kuelekea moja kwa moja Bulawayo, utakapochezwa mchezo huo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STRAIKA NA MIDO HATARI PLATINUM WALIOIKOSA YANGA DAR, SASA WAPO FITI KWA MCHEZO WA MARUDIANO JUMAMOSI MANDAVA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top