• HABARI MPYA

    Wednesday, April 01, 2015

    WANA MWANZA IPIGIENI `SALUTI` TFF, REKEBISHENI HAYA

    Na, Hemed Kivuyo, DAR ES SALAAM
    NILIPOFIKA Mwanza  nilikumbuka wimbo wa Marijani Rajabu unaoitwa `Mpenzi Aisha`. Marijani enzi za uhai wake alifika Mkoani Mwanza akakutana na msichana aitwae Aisha,walipendana na wakakubalina kuwa Aisha atakuja Dar es salaam kwa Marijan na kisha wapange mipango ya Ndoa.
    Miezi michache baadaye Aisha alipelekwa Nchini Uingereza na Wazazi wake kwaajili ya masomo. Marijani alimsubiri Aisha bila mafanikio. Akaandika mashairi na kutunga wimbo `Mpenzi Aisha` bado nakusubiri,natamani kukufuata na kazi zinanitinga,bado nakusubiri.
    Asubuhi ya jumapili  siku ambayo timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa stars) ilicheza na timu ya Taifa Ya Malawi nilikutana na Mmiliki wa chombo hiki cha Habari ( Bin Zubeir) hukohuko Mwanza,alinipeleka mahali akaninunulia Supu ya samaki na samaki mwenyewe. ( acha bwana ,,acha kabisa,,supu kama imewekwa nazi!!!)
    Lakini Kikubwa ilikuwa ni kufuatilia mchezo kati ya Taifa stars na Malawi uliyopigwa uwanja wa  ccm Kirumba na kutoka sare ya 1-1.

    Ingawa asubuhi yake kulikuwa na `kamvua` lakini hamasa ilikuwa kubwa kwa wana mwanza,walijaa uzalendo kwa timu yao ya Taifa,kadiri muda ulivyokwenda walizidi kuingia uwanjani kuangalia timu yao ya Taifa.
    Mpaka mchezo unaanza mamia ya wana Mwanza walikuwa katika foleni ya kuingia Uwanjani.
    Wakati mpira ukikaribia kuanza timu zikiwa zinapasha kulikuwa na muziki mkubwa,niliusikia wimbo wa Dk Remmy ``Mwanza oohh Mwanza,,mwanza tutarudi tenaaa..mwanza Mji mzuri``. Ni Kweli Mimi Binafsi Nitarudi tena Mwanza.
    Mashabiki walikuwa wakiimba wimbo wa Taifa la Tanzania kila wakati.
    CCM Kirumba ni uwanja mzuri uliyostahili kuchezwa mchezo wa ligi kuu na hata wakimataifa kama ule,huwezi kuufananisha na uwanja wa mkwakwani unaochezewa ligi kuu kwa kulazimishwa tu.
    Mara kwa Mara Timu ya Taifa hucheza Michezo yake Uwanja wa Taifa,hivyo wakazi wa Dar es salaam walishaizoweya Timu yao ya Taifa na hata wengine walikuwa wanauwezo wa kubuni kikosi na wakapatia. Inawezekana hata mtu wa Mwanza akaweka kutabiri hivyo lakini si kwakuona.
    Ilikuwa ni Fursa nzuri kwa wana Mwanza ambao wapo wengi sana wanaopenda Mchezo wa Soka. Hamasa na uzalendo uliyoonyeshwa na watanzania wa Mwanza kwa timu yao ya Taifa sikuwahi kuona ikifanyika Uwanja wa Taifa. Wengine walivaa mavazi yenye Nembo ya Taifa la Tanzania.
    Nasema hivyo lakini sitaki kuamini kama mashabiki wa Soka wa Dar es salaam wameishiwa Uzalendo kiasi cha kuzidiwa na mashabiki wa Mwanza.
    Lakini niwape Kongole wana Mwanza kwa uzalendo waliyounyesha kwa Timu yao ya Taifa.yupo mtu mmoja wa Mwanza anaitwa Harun Popat alisimama Nyuma yangu,muda wote alikuwa akishangilia huku akipaza sauti ya kizalendo kwa wachezaji wa Stars. Aliakisi wana mwanza wengine wengi kama yeye.
    Shirikisho la Soka Nchini TFF lilikuwa na mamlaka ya kupeleka Mchezo huo mkoa mwingine na siyo Mwanza,Lakini liliamua kupeleka Mwanza. Sijajua sababu zao lakini kimsingi mimi nadhani walikuwa sahihi katika maamuzi yao.
    Pamoja na kuwa na Uwanja wa ccm kirumba ni uwanja mzuri lakini hawakuweza kuona Ligi kuu ya Tanzania Bara ikipigwa uwanjani hapo,pamoja na kuwa Mwanza ina historia ya kutoa wachezaji mahiri waliyoitumikia timu ya Taifa kwa umahiri mkubwa miaka ya Nyuma lakini walikosa Burudani ya Soka kwa kipindi kirefu. Toka ilipotoweka timu ya  Pamba.
    Kwakuwa TFF ilikuwa na uwezo wa kupeleka mchezo huo popote hivyo basi wapenda Soka wa Mwanza ni dhahiri wanapswa kushusha pumzi na kusema ahsante TFF`` kwakutukumbusha mbali.
    Hii Ni funzo kwa viongozi wa Soka Mkoani Mwanza kuhakikisha wanakuwa na timu zaidi ya mbili zinazoshiriki Ligi Kuu ili kurejesha  hamasa ambayo huonekana pindi TFF inapopeleka mchezo kama huo Kirumba. Mpandeshe Timu nyingine sioyo kwa huila bali uwezo kwakuwa naamni Mwanza kuna Vipaji kama vya akina Juma Amiri vingi tu.

    UWANJA NA MAZINGIRA YAKE.
    Pamoja na kuwa mazingira ya Ndani ya Uwanja siyo mabaya lakini upande wa majukwaani inahitajika uboreshaji . Pia katika Uingiajia wa Uwanjani watazame upya kwakuwa ni mageti mawili tu hutumika. Hivyo umati unapozidi kuongezeka na usalama nao utazidi kuwa mdogo,watoto na walemavu nao watakosa haki yakuingia uwanjani.
    Sikuona sehemu maalum ya waandishi wa Habari kukaa,kadhalika eneo la vyumba vya wachezaji ni mbali kutoka Uwanjani. Yaani Mchezaji anatoka katika `Benchi` anatembea kupitia katikati ya uwanja ili aende katika vyumba vyao .
    Wakati unaingia katika Vyumba hivyo  kabla hujaingia ndani juu kuna mabati magumu ambayo huonyesha Nyufa na hupiga kelele pindi mashabiki wanapopita juu. Hivyo huatarisha usalama wa wachezaji na waalimu wao.
    Ni afadhali uongozi wa Uwanja huo ukatazama upya utaratibu kama ikiwezekana kujenga vyumba vya wachezaji chini ya Jukwaa kuu lenye bati. Pia kuwe na eneo maalum la waandishi wa Habari.
    Kuchezwa Mchezo huo mkubwa katika uwanja wa Kirumba kuwakumbushe viongozi hao kuondoa kasoro hizo kwakuwa mtaangalia Ligi Kuu sasa msimu unaofuata.
    TIMU YA TAIFA- TAIFA STARS
    Kadiri miaka inavyokwenda tunaanza kufuata misingi imara ya Mwalimu kuachiwa afanye kazi yake bila kuingiliwa. Kikosi kilichopangwa na Mwalimu Mart Nooj kinadhihirisha uhuru aliyopewa. Aliwapa nafasi wachezaji kadhaa ambao hawapati nafasi ya kudumu katika vilabu vyao. Ingalikuwa miaka ya Nyuma angepewa `ujumbe` wee hebu tupangie hawa tuliyowazoweya`.
    Nooj aliwapa nafasi wachezaji hata ambao hawaaminiki katika vilabu vyao ( nitawataja makala ijayo)
    Lakini kupewa uhuru kwa Mwalimu wa Stars isimpe sababu ya kufanya  utetezi wa rekodi yake bila kuangalia madhara ya kutopanda kwa timu ya Taifa.
    Kuna wachezaji kadha ambao wameonyesha uwezo mkubwa katika vilabu vyao na nafasi wanazocheza na Nooj amewaona kwakuwa anaangalia michezo mingi ya Ligi Kuu.
    Nitatoa mifano Michache,Beki  wa kushoto,yupo mtu kama Mohamed Hussein wa Simba,huyu ameonyesha uwezo mkubwa kuliko huyo Beki  ambaye Nooj anamtumia kwasasa.
    Kuna mifano mingi iliyo hai ambayo huonyesha Nooj anataka kulinda Rekodi yake zaidi kuliko kuangalia uhai wa baadaye wa Timu yetu ya Taifa. Nasema hivyo simaanishi TFF Imefanya kosa kumpa uhuru huo. Laa hasha!
    Watu wa Dar Es Saala na kwingineko tuwaige watu wa Mwanza kwa Uzalendo
    (Mwandishi wa makala haya ni mtangazaji wa Redio One na ITV, ambae anapatikana kwa namba +255 655 250157 na +255 752 250157)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WANA MWANZA IPIGIENI `SALUTI` TFF, REKEBISHENI HAYA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top